Waters of Life

Biblical Studies in Multiple Languages

Search in "Kiswahili":
Home -- Kiswahili -- John - 081 (Jesus washes his disciples' feet)
This page in: -- Albanian -- Arabic -- Armenian -- Bengali -- Burmese -- Cebuano -- Chinese -- Dioula? -- English -- Farsi? -- French -- Georgian -- Greek -- Hausa -- Hindi -- Igbo -- Indonesian -- Javanese -- KISWAHILI -- Kyrgyz -- Malayalam -- Peul -- Portuguese -- Russian -- Serbian -- Somali -- Spanish -- Tamil -- Telugu -- Thai -- Turkish -- Twi -- Urdu -- Uyghur? -- Uzbek -- Vietnamese -- Yiddish -- Yoruba

Previous Lesson -- Next Lesson

YOHANA - Nuru inaangaza gizani
Somo la Injili ya Kristo kufuatana na Mtume Yohana
SEHEMU YA 3 - Nuru yang’aa ndani ya shirika la Mitume (Yohana 11:55 - 17:26)
B - Mambo yaliyofuatana na chakula cha Bwana (Ushirika utakatifu) (Yohana 13:1-38)

1. Yesu aosha miguu ya wanafunzi wake (Yohana 13:1-17)


YOHANA 13:1-5
“Basi, kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali akijua ya kuwa saa yake imefika, atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, naye ali amewapenda watu wake katika ulimwengu, aliwapenda upeo. Hata wakati wa chakula cha jioni; naye Ibilisi amekwisha kumtia Yuda, mwana wa Simoni Iskariote, moyo wa kumsaliti; Yesu, hali akijua ya kuwa Baba amempa vyote mikononi mwake, na ya kuwa alitoka kwa Mungu naye anakwenda kwa Mungu, aliondoka chakulani; akaweka kando mavazi yake, akatwaa kitambaa, akajifunga kiunoni. Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga.”

Kuanzia sura hii Yohana anasogea kwenye hatua na jambo jipya la injili yake. Kabla ya hapo, Yesu alikuwa anawaita watu kwa jumla; tukisoma kwa kusikitika maneno hayo, “Nuru yaling’aa gizani, wala giza halikuiweza.” Maneno hayo yalithibitika kwao. Je, basi, Yesu alishindwa? Hapana ! Kwa vile watu kwa jumla hawampokei, basi Bwana aliwachagua wachache waliokuwa tayari kwa kuungama, akawakusanya katika shirika la wanafunzi wake. Katika sura zifuatazo tutasoma jinsi Yesu alivyosema na hao wachaguliwa; aliongea nao kama bwana-arusi anavyosema na bibi-arisi wake. Yeye ni wao, jinsi wao walivyo wake. Upendo wa Mungu ikawa ndiyo shabaha ya maongeo yao. Upendo huo siyo namna ya kujisikia mwenyewe, inadokeza wito wa huduma. Ndani ya Biblia upendo unahusisha namna ya kujitoa kwa unyenyekevu kwa ajili ya wale wasiostahili. Katika maongeo hayo Yesu anafunua sifa zake za ndani na za maana sana kwa wanafunzi wake, alieleza upendo wake katika mfano wa mtumishi, akifananisha maisha yake, kifo na kufufuka kwake na mtumishi wa Mungu.

Yesu aliwafundisha kwamba atakufa kabla ya Pasaka iliyokuwa karibu. Alikuwa akirudi kwa Bvaba yake. - Je, mwelekeo huo ni wa kwako pia? - Yesu alikuwa ulimwenguni, lakini macho yake daima yalimwelekea Baba yake. Kutoka kwake alipokea nguvu, uongozi na furaha aweze kuvumilia watu waovu kama wale. Kwa ushirikiano na Mungu naye aliona kwamba Shetani alinong’oneza moyoni mwa mmoja wa wanafunzi wake mawazo ya upotovu. Huyu mtu polepole alijifunua kwa choyo, kiburi na chuki. Hata hivyo, Yesu hakumchukia msaliti wake, bali alimpenda kwa upendo tukufu hadi mwisho.

Yesu hakumwelekea msaliti vivi hivi, kana kwamba tukio hilo ilipasa kutokea tu. Si Yuda, wala Kayafa, Herode, Pilato au viongozi wa Wayahudi pamoja na umati wa watu wao waliokuwa wenye kuamua yatakayotokea, lakini kwa sababu ya kuingia kwake kabisa ndani ya ubinadamu pamoja na utii wake, Baba alikabidhi roho zote pia na wanadamu wote kwake.

Yeye aliamua afe kama Kondoo wa Mungu naye akapanga ratiba ya matokeo. Tangu mwanzo hata mwisha wa dhoruba ya matokeo hayo, yeye hakupoteza uwezo wa kuona alikotoka na shabaha ya mbeleni. Yesu ndiye Bwana, ndiye ageuzaye mwenendo wa historia.

Kristo hakutamani tu kurudi kwa babaye juu, lakini aliwavuta wanafunzi wake ndani ya ushirikiano wa raha njema ya Mungu. Aliwafundisha na mfano wa unyenyekevu, akionyesha mbele zao upendo tukufu kwa namna ya utendaji. Basi hivyo akawa mtumishi; akajichukulia maji na kupiga magoti mbele za wanafunzi wake, ili atawadhe miguu yao na kuikausha. Alijifanya kuwa wa mwisho wa wote, ili hata aliye wa chini kabisa kati yao aweze kutambua kwamba, Mungu ameamua kuhudumia binadamu. Bwana hatawali kwa namna ya baridi na bila kujishughulisha, bali anpiga magoti kwa ajili ya kuwasafisha na kuwabadilisha katika mfano wa upole wake.

Yesu ndiye kielelezo chetu cha juu sana. Ni lini tutakapoinama mbele zake na kumwabudu? Lini tutabadilisha nia zetu na kupinda migongo yetu iliyonyoka na ugumu mno? - Ndugu, kwa wakati wote unapokataa kuvunjika, bila kuwahudumia ndugu zako na bila kuwapenda adui zako, au bila kufunga vidonda vya walioumizwa, basi hujawa Mkristo wa kweli. Je, wewe unatenda kama mtumishi au kama bwana (boss)? Kumbuka, Yesu ndiye mtumishi wa wanadamu wote, anainama chini kuwahudumia wote, pia na wewe. Utapokea huduma hiyo au kujihesabu mwenyewe kuwa na majivuno, kwamba u mwema na bila haja na huduma ya Mungu?

YOHANA 13:6-11
„Hivyo yuaja kwa Simoni Petro. Huyo akamwambia, Bwana! Wewe wanitawadha miguu mimi? Yesu akajibu, akamwambia, Nifanyalo wewe hujui sasa; lakini utalifahamu baadaye. Petro akamwambia, Wewe hutanitawadha miguu kamwe. Yesu akamwambia, Kama nisipokutawadha, huna shirika nami. Simoni Petro akamwambia, Bwana, si miguu yangu tu, hata na mikono yangu na kichwa changu pia. Yesu akamwambia, Yeye aliyekwisha kuoga hana haja ila ya kutawadha miguu, bali yu safi mwili wote; nanyi mmekuwa safi, lakini si nyote. Kwa maana alimjua yeye atakayemsaliti; ndiyo maana alisema, Si nyote mlio safi.”

Wanafunzi walikuwa wamehangaishwa na kazi ya Bwana wao kuwaosha miguu yao. Kama wangalifahamu atakalofanya baada ya “Chakula cha Bwana”, wangaliosha miguu yao wenyewe mara moja. Bwana wao hakufanya tu Agano Jipya kati yao na Mungu, bali aliwaonyesha na yaliyomo na maana ya Agano hilo: Maana yake ni kufanya yote kwa upendo na unyenyekevu, hasa pamoja na kuhudumia kwa matendo.

Petro alikuwa mwenye bidii na kujitokeza zaidi ya wanafunzi wenzake. Hakupenda kuhudumiwa na Yesu; hivyo akajaribu kuzuia kutawadhwa, na bila kujali maneno ya Bwana wake kwake. Ndipo Yesu alieleza hiyo siri ya kutawadha miguu kwa wanafunzi wote, kana kwamba anayaeleza hata kwetu, “Bila kuoshwa hamna shirika katika ufalme, na bila msamaha wa dhambi hamwezi kudumu ndani yangu.” Kuoshwa ndani ya damu yake ni siku zote, na kudumu katika hatua za kusafishwa inaendelea daima. Ni yeye mwenyewe anayekuongoza katika neema, akikutunza ndani ya ushirikiano na Mwana wa Mungu.

Hapo basi, Petro naye akaona nuru, na kwa kuangalia mikono yake yenye kutenda mabaya, na kwa kutafakari uvivu wa akili yake kutambua mipango ya Mungu, akaona aibu na kuomba kuongezewa kuoshwa hadi kusafisha mwili wote. Basi, Yesu akamhakikishia hivyo: “Mtu akija kwangu atatakata, tena kikamilifu katika msingi wa kifo changu.” Hapo tunajifunza na sisi kwamba hatuhitaji kusafishwa kipekee au kuongezewa utakatifu, maana damu ya Yesu inatusafisha na dhambi zote kabisa. Hakuna utakatifu kubwa zaidi au kikamilifu zaidi kuliko kusamehewa dhambi zetu kwa damu yake. Jinsi tunavyokusanya vumbi kila siku kwa kutembea hapo na pale, tuko tunaomba kila wakati, “Utusamehe makosa yetu yote.” Wakati huo watoto wa Mungu wanahitaji kila siku kuosha miguu yao tu; watoto wa dunia hii wanahitaji kusafishwa kabisa maisha yote.

Yesu aliwaangalia wanafunzi wake na kusema, “Ninyi mmekuwa safi.” Aliwaalika kuingia katika Agano na Mungu. Kondoo alikufa kwa ajili ya wanafunzi wake, ili kuwafanya wapime namna ya kudumu katika ushirikiano huo tukufu. Hakuna mwanadamu aliye safi ndani yake, lakini damu ya Yesu hutusafisha na dhambi zetu zote.

Ni sikitiko kwamba, si wote wa wafuasi wake waliokuwa takatifu, na ndivyo ilivyo na leo. Baadhi yao hufanya huduma ya midomo tu kwa kusafishwa hivyo kimsingi, na wanajifanya kana kwamba wanaiamini damu ya Kristo, lakini Roho Mtakatifu hajawa akiwajaa. Roho ya Shetani anachochea chuki, wivu, kiburi na uzinzi ndani yao. Hivyo kati ya wacha Mungu mara kwa mara utawakuta wale waliopagawa na roho chafu na upendo kwa pesa. Yesu atamani kuosha miguu yako kila siku na kukuweka huru na aina zote za dhambi, na kukusafisha kwa taratibu, ili ukafaa kwa ushirikianao na Mungu. Ujipime mwenyewe, je wewe ni mtumishi au bwana (boss)?

SALA: Bwana Yesu, tunakushukuru sana kwamba uliacha kabisa utukufu wako na kuja chini kwetu tulio wachafu. Ulijishusha chini, ili kuosha miguu ya wanafunzi wako, na pia ulitakasa mioyo yetu na dhambi zote. Tunakuabudu tukikusihi sana utuweke huru na mawazo yote ya kiburi, ili tuweze kuinama chini na kufanywa watumishi wako. - Nisaidie nikubali kuwa wa mwisho katika wote, na niwe tayari kukuhudumia katika kanisa na familia yangu.

SWALI:

  1. Bwana Yesu kutawadha miguu ya wanafunzi wake ilikuwa na maana gani?

YOHANA 13:12-17
“Basi alipokwisha kuwatawadha miguu, na kuyatwaa mavazi yake, na kuketi tena, akawaambia, Je! Mmeelewa na hayo niliyowatendea? Ninyi mwaniita Mwalimu na Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo. Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi. Kwa kuwa nimewapa kielelezo, ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo. Amin, amin nawaambia ninyi, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka. Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda.”

Yesu hakuanza maongezi yake ya kuwaaga kwa maneno matupu tu. Mara nyingi maneno kama hayo yafaa kidogo tu, yasipobebwa na utendaji. Yeye aliwauliza wafuasi wake, kama wameyashika maana ya kazi yake ya mfano kwao, “Fungueni macho yenu na kuona, mimi nipo pamoja nanyi kama mmojawenu. Sikujiketisha juu yenu kwenye kiti cha enzi, ili ninyi mtambae mbele yangu kama watumwa. Hapana! Nimejivua utukufu wote na kuwa mmojawenu. Zaidi ya hapo, nimeacha mahali pangu kama mwalimu na bwana, ili niwe mtumishi. Mmeelewa sasa mwelekeo, ambao upendo tukufu unapasa kushika? Mwenye kiburi anajivuna, mwenye upendo anajinyenyekeza na kuvumilia mambo yote, hujikana na kuhudumia kimwili na ki-matendo.”

“Mnapenda kuwa wanafunzi wangu, jinsi nilivyo kielelezo kwenu; mimi siwaambii tu, bali naitendea kazi kule kufundisha kwangu. Mnitazame: Mimi ni mtumishi. Mkipenda kunifuata, mwinameni chini na kutendea huduma ninyi kwa ninyi. Yule kati yenu apendaye kuwa wa kwanza, ndiye mwenye udhaifu zaidi. Lakini yule anayehudumia wengine kwa upole na kudumu chini, ndiye mkubwa kweli.”

“Msidhani kwamba Kanisa ni mkusanyiko wa watakatifu kamili. Wote wamo katika mfuatano wa kuimarika. Nimewatakasa wote nao ni watakatifu kwa daraja. Lakini kila mjumbe anahitaji uvumilivu na muda aweze kukua kiroho. Pia kila mmoja hukosea na kujikwaa. Hapo nawapa uamuzi na agizo langu: Msameheane ninyi kwa ninyi makosa na dhambi. Msihukumane, bali msaidiane. Msioshe vichwa vya vya wengine, bali miguu yao. Yeyote asitawale juu ya wengine; maana ninyi ni ndugu. Kama mtatenda hivyo, mtatambua yale ambayo nimekwisha kuyaweka wazi mbele yenu: Sikuja kuhudumiwa lakini kuhudumu. Maisha yangu yote ni huduma, sadaka na kujitoa kwa wote.”

“Nawatuma ulimwenguni kuwa mitume wa upendo. Anayetumwa ni mkubwa sawa na yule amtumaye. Huduma yenu ya kwanza ni kubadilika kuwa watumishi kama mimi. Mkitambua hayo, mtakuwa mmeshika vizuri shabaha na lengo la Ukristo.“

„Kanuni yangu ya pili: Mkiyajua hayo, heri mkiyatenda. Sikuzungumza habari ya upendo kwa maneno tu, nimeyatendea kazi.“ Huduma maana yake ni kazi na kujitoa, sio maneno, sala na kujisikia tu. Msukumo wa kuhudumia ni ndani ya namna ya mwumini. Kutoka kwa chanzo hiki hujitokeza matendo mbalimbali ya upendo. Asiyekuwa tayari kuhudumu, kwake ni vigumu kuwa mwumini. Maombi hata ya kulia kabisa yasipokuwa na matendo yafuatayo, basi ni unafiki tu. Wewe hukuokolewa kwa matendo mema; ni damu ya Kristo iliyokuokoa. Lakini ukijishusha kwa wadhaifu na wanaopotea-potea na kuwahudumia kwa uvumilivu, utajazwa na furaha ya Mungu. Upendezi mwema wa Mungu huwafunika watumishi wa kweli wa Kristo.

Ndugu, unatamani kuwa bwana na mwalimu? Umwangalie Yesu. Yeye ndiye Mwalimu kweli kweli. Na hapo anasimama mbele yako akiwa mtumishi. Je, unapenda kutendea kazi mafundisho yake? Anza leo hii ukahudumu. Umwombe katika sala zako, ni wapi, na namna gani, na ni nani anapenda umhudumie. Ukipata kufahamu hayo, heri ukiyatenda.

www.Waters-of-Life.net

Page last modified on September 01, 2014, at 04:36 PM | powered by PmWiki (pmwiki-2.3.3)