Waters of Life

Biblical Studies in Multiple Languages

Search in "Kiswahili":
Home -- Kiswahili -- The Ten Commandments -- 05 -- Third Commandment: Do Not Take the Name of God in Vain
This page in: -- Afrikaans -- Arabic -- Armenian -- Azeri -- Baoule -- Bengali -- Bulgarian -- Cebuano -- Chinese -- English -- Farsi -- Finnish? -- French -- German -- Gujarati -- Hebrew -- Hindi -- Hungarian? -- Indonesian -- KISWAHILI -- Malayalam? -- Norwegian -- Polish -- Russian -- Serbian -- Spanish -- Tamil -- Turkish -- Twi -- Ukrainian? -- Urdu? -- Uzbek -- Yiddish -- Yoruba

Previous Lesson -- Next Lesson

TOPIC 6: AMRI KUMI - Kuta za ulinzi wa Mungu zinazolinda wanadamu wasianguke
An Exposition of the Ten Commandments in Exodus 20 in the Light of the Gospel

05 - Usilitaje Bure Jina La Bwana, Mungu Wako



KUTOKA 20:7
“Usilitaje bure jina la Bwana, Mungu wako, maana Bwana hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure.”


05.1 - Jina la Mungu

Mwanadamu hawezi kuishi bila Mwumbaji wake. Aliumbwa katika sura ya Mungu, lakini alimwacha (aliondoka kwake). – Tangu hapo ametangatanga katika jangwa la dunia hii, akitafuta-tafuta nyumbani kwake iliyopotea na kutamani kuiona asili yake iliyojificha. Mwanadamu tangu hapo amejaribu kutengeneza maelfu ya miungu mingine, ambazo nyuso zao za kutisha zinaonyesha hofu za mtu asizozitamka, pamoja na tamani zake. Hutumia fedha kwa ajili ya vipindi vya uganga, kutabiri mistari mkononi na maaguzi kwa nyota, ambazo zote hazileti ulinzi kwa mabaya. Waislamu hubusu lile jiwe jeusi kwa heshima kana kwamba kuna roho toka mbinguni ndani yake. Wabudhisti huabudu lile sanamu kubwa la dhahabu ya Budha, linalocheka bila kupendelea kwa wafuasi wake wasiotambua lolote kiroho.

Ufunuo wa moja kwa moja wa Bwana juu yake mwenyewe anapotamka, “Mimi ndimi Yehova, aliye Bwana”, basi lingekomesha kazi ya watu kutafuta-tafuta. Kutokea kwake ndani ya kichaka kilichowaka moto bila kuteketea kulikuwa ya kihistoria, maana Bwana alijijulisha kwa Musa na kueleza jina lake. Haya, kuna mafunuo kadhaa ya Mungu katika mfululizo wa Agano la Kale na la Agano Jipya. Biblia hutupatia majina na sifa 638 kwa ajili ya Mungu wa Utatu. Kwenye lugha za kishemu (kiyahudi, kiarabu n.k.) kila sifa linatajwa kwa jina lingine.

Hivyo, Mungu sio mtenda haki tu, lakini mwenyewe ni Mhaki; ambaye ndani yake haki zote zimejumlika. Yeye si mtakatifu tu, lakini yeye ndiye Mtakatifu ajaaye utakatifu wote. Katika majina hayo kila moja ni mwali wa nuru ya utukufu wake. Hata hivyo jina lile litokealo mara nyingi kuliko mengine yote ni Yehova, (mara 6,828 ndani ya Agano la Kale). Na maana ya jina hilo ni Mtunzaji mwenye enzi yote, Mtakatifu, Asiye na Kosa, Bwana wa historia, ambaye hajabadilika, wala hatabadilisha uaminifu wake.


05.2 - Bwana ndani ya Agano Jipya

Bwana mwenyewe alizaliwa kuwa mwanadamu ndani ya mwili wa nafsi ya Yesu wa Nazareti, inavyoelezwa ndani ya Agano Jipya. Malaika, manabii na waumini wote hukiri na kukubaliana kwamba, “Yesu ni Bwana”. Hata hivyo Yesu hakujitukuza mwenyewe, bali kila wakati alimheshimu Baba yake wa mbinguni. Kwa kweli, alitufundisha sala hii, “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe.” Katika sala hii jina la Baba linaheshimiwa, linatukuzwa na kutakaswa mbele na juu ya majina yote mengine. Ufunuo wa Mungu Baba kwa njia ya Yesu ulituinua kwenye hali ya juu kuhusu ufahamu wa Mungu.

BwanaYesu kweli alikuwa ni unyenyekevu mwilini. Yeye alikamilisha upatanisho kati ya Mtakatifu na wenye dhambi wote kwa njia ya kifo chake kwenye msalaba wa aibu. “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani,na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba” (Wafilipi 2 : 9-11). Roho Mtakatifu alikuwa akitukuza jina la awali la Yesu tangu milele, naye atuhakikishia kwamba YEYE ndiye “BWANA”. Wakati uo huo Roho Mtakatifu anatuthibitishia habari ya umoja wa Mungu aliye Baba, na ya Mwana na ya Roho Mtakatifu. Umoja wa upendo kwa ukamilifu hutuonyesha ile asili ya Mungu wetu. Mfalme Daudi alikuwa amewahi kusikia ufunuo huo akitamka katika Zaburi ya 110:1 : “Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako.”


05.3 - Je, ina maana gani kufahamu jina la Mungu?

Mtu fulani anapoingia ndani ya mji geni, atashukuru akiwa na anwani ya mtu anayemfahamu mle. Ataweza kwenda kwa jamaa huyu na kumwuliza uongozi na msaada. Heri mtu yule ajuaye jina la kweli la Mungu na kutunza „namba ya simu yake“ (Zaburi 50:15): „Ukaniite siku ya mateso; Nitakuokoa, na wewe utanitukuza“. Bwana wetu aliye hai mbinguni halali, naye kwa hamu hungojea simu zetu za kiroho.

Kila tunapokutana na Mungu wetu Mtakatifu, unafunuliwa kwa uwazi kabisa uhusiano wetu ndani ya makosa, upweke na upotevu wetu. Enzi ya utukufu wake unaweka wazi uadilifu wetu wa juu juu tu, pia na kuonyesha utu-wema wetu ulivyo bovu. Bali rehema za Mungu unatutia moyo kukiri makosa yetu, na unyenyekevu wake utaonyesha wazi kiburi chetu kilivyo kama sumu. - Kufahamu jina la Mungu kunawezesha watu waliovunjika kimoyo waweze kujaliwa uhusiano wa binafsi na Mungu.

Imani yetu inapoongezeka ndani ya Mungu inatuwekea mizizi ndani ya Amri ya tatu anaposema, „Mimi ndimi Bwana Mungu wako“, ambamo neno lile la kutamka „wako“ linadokeza kwamba Mungu aliye Mtakatifu anajifungamanisha na viumbe vyake, walio watenda dhambi, wasiostahili na wadhaifu. Huwahakikishia habari ya uaminifu na utunzaji wake. Kufuatana na Agano Jipya, hutuingiza hata ndani ya familia ya Mungu, ambamo Yesu ndiye kichwa, na sisi tu viungo watenda kazi ndani ya mwili wake wa kiroho.

Mungu Baba atamani kuwa na nia moja na roho moja na watoto wake na kufanya kazi kwa njia yao kuokoa kizazi hiki kiovu. Ndani ya Rehema zake, awajalia fursa ya kumtegemea na kutenda kazi katika jina lake.


05.4 - Kutumia Jina la Bwana bure (ovyo)

Twaishi ndani ya ulimwengu unaoongozwa kwa kina na mafunuo ya Mungu ndani ya Biblia. Hata hivyo, ni watu wachache wanaomtegemea Mungu kwa moyo wote. Mwanadamu asipodumu usoni pa Mungu, ataishia katika hali ya kutumia jina la BWANA bure. Watu kama hawa wanamtumia na mashaka au wasiwasi, kana kwamba wanafanya malipo na fedha isio na thamani. Hata wakristo waliozaliwa mara ya pili wako hatarini kumhuzunisha Roho Mtakatifu kwa maongezi yao maovu. Wanaongea bila kutafakari habari ya kutaja jina la Mungu. Amri ya Tatu inatuonya na kutaka kutuzuia tusitamke jina la Bwana ovyo.

Wakristo wa majina tu hutamka jina la Mungu bila kukoma, lakini kwa kutokutafakari wanaposema, “Ee Mungu!” au “Kwa Mungu!” na kadhalika. Wanafanya kama watoto wanaocheza na simu, wanachagua namba, lakini bila kusema na yule waliompigia, anayefanya hima kujibu wito wa simu. Ni wazi kwamba, wakiendelea kufanya hivyo tena na tena, yule anayepigiwa atapata hasira na kuacha kusikiliza simu hiyo inayomsumbua tu. – Mungu husikiliza tunapomwita katika sala. Je, unafikiri mambo gani, wakati unapotamka jina lake? Unapotumia jina lake bila kutafakari, basi unaonyesha jinsi maisha yako unayoishi ni kwa sehemu ndogo tu mbele za Bwana wako.


05.5 - Waislamu wanavyotamka jina la Allah

Kila Mwislamu anatakiwa kutamka jina la Allah mara nyingi, akitumaini kwamba atahesabiwa haki na kuonekana kuwa wa kutegemewa, mwenye haki na mwaminifu. Ataamini kwamba kadiri anavyorudia kutamka jina la Allah, ndivyo dhambi zake zitakavyosamehewa. Basi wazo hilo likasukuma namna hiyo ya kuabudu juu juu tu, ambayo kutaja jina la Allah ovyo ikapata kuwa sehemu ya ibada. Ni muhimu kuelewa hapo kwamba, Mwislamu hana uhusiano wa binafsi na Allah. Kumsema Allah ni kama kumumunya kwa mtumwa kumwitikia bwana wake mwovyo, ambaye hawezi kujua kama anasikiliza au la.

Zaidi ya hapo, sala zake za kila siku ni mazoea yaliyoandikishwa. Mwislamu wa kawaida anatakiwa kurudia Fatiha (Sura al-Fatiha) mara kumi na saba, kwa ukimya au kwa kusikika, katika mfululizo wa sala zake mara tano kila siku. Karibu millioni elfu moja ya Waislamu wanapaswa kusali Fatiha kwa kiarabu kote ulimwenguni, ingawa zaidi ya millioni mia nane kati yao hawaelewi kiarabu. Inasikitisha kwamba, hata Sala ya Bwana hurudiwa bila mawazo kwa watu wengi hata makanisani kwenye ibada.


05.6 - Sala zenye mashaka na hoja zisizofaa

Si Waislamu tu wanaorudia kawaida zao za dini bila kufikiri, lakini hata Wakristo pia wasiohesabika husema sala zao kama mama fulani anayeimba kwa mtoto wake anapoenda kitandani alale. - Tunawezaje kuthubutu kumwita Mungu bila kutazamia jibu kutoka kwake, au kusema na Mungu wakati tunapowaza habari ya biashara yetu au mengine madogo? Ikiwa kwa mfano, tungepata nafasi ya kukutana na Mkuu wa nchi yetu mwenyewe na kuzungumza naye binafsi, je, tusingetafakari mapema juu ya kila neno na kulipima kabla ya kulitamka? Na je, umuhimu wa Mungu kwetu unapungua kuliko kwa mwanadamu? Mtu anapoomba bila kutafakari, basi anamdharau Mungu.

Wana-theologia mara kwa mara hufikia ukingoni kwa kutendea jeuri Amri ya Tatu na kumhuzunisha Roho Mtakatifu wanapochunguza Biblia na kujadili tabia na matendo ya miujiza ya Mungu kana kwamba wanajadiliana majaribio fulani ya kisayansi ya uvumbuzi, wala hawasikii kuwepo kwake Mungu kwenye kuhojiana juu ya Neno lake. Maana Mungu siye wazo au kitu fulani. Yeye ni Nafsi aliye hai na yupo nasi kila wakati. Husikiliza maongezi yetu na kutambua mawazo yetu kutoka mbali. Kwa sababu hiyo, uchunguzi wowote wa ki-theologia unaopungua hofu ya Mungu na kicho chake basi, bila mashaka utaongoza kwenye hatua ya kutendea jeuri Amri ya Tatu.


05.7 - Kutumia Jina la Mungu kwa hali ya dhambi

Ole kwake apindaye Neno la Mungu kwa kusudi, alitumiaye kwa mzaha au kulicheka ! Wafanyao hayo wanalishutumu Jina lililo juu ya kila jina na kutokuonyesha hofo au heshima mbele zake. Kwa hiyo, kwa vyovyote tusiungane na watu wanaocheka juu ya Neno la Mungu. Badala yake, tungewaonya wachokozi hao na kusimama kwa kumtetea Mungu. Wenye kuandika vitabu au kutunga filamu wanaelewa matokeo muhimu sana ya maneno ya kidini wanapoyatumia katika matoleo yao. Hata hivyo hawatumii maneno kama „dhambi“, „jehanum“ au „kupotea“ kwa maana yao hasa; wanayajaza na maana ya kawaida ya dunia. Lakini maneno yao yatawarudia na kuwahukumu siku moja.

Watu mara kwa mara hupata hasira juu ya wengine, na katika ghadhabu yao, ndipo wanalaani kwa maneno kama „Mungu“, „Allah“ au „Yesu“. Wanaapa au kusema habari ya adhabu ya Mungu au mambo mengine ya kidini bila kuyatafakari. - Siku moja mchungaji alikutana na mjenzi na kusikia jinsi alivyoapa na kulaani, basi akamwuliza, „Je, wewe kila wakati unasali kwa sauti kubwa namna hii?“ Yule mtu alichanganyikiwa kidogo na kuitika kwa nguvu, „Sikuwa nasali.“ Basi mchungaji alimjibu, „Lakini nimekusikia ukiitia jina la Mungu, na kwa kweli atakujibu.“ Huyu mfanya kazi alisimamishwa katika matamshi yake.

Mara nyingi tu watu hutumia maneno ya kuapa kwa juu juu tu dhidi ya mtu mwingine hata awe ni jamaa yake. Chuki ya ndani sana ndiyo sababu ya maneno hayo. Yesu huhesabu laana za namna hiyo kuwa sawa na uuaji, kwa sababu zinachafua sura ya Mungu ndani ya mtu.


05.8 - Onyo la Mungu: Adhabu kali

Kuna onyo zito kwenye Amri ya tatu, „Mungu atamwadhibu bila huruma yeyote atakayetumia Jina lake ovyo.“ Ingawa kuna onyo hilo kali, watu wengine hutamka jina la Mungu hata kufunika kazi fulani baya na wanatumia jina lake kwa kusudi ya kutakasa tendo lao ovu. Ole kwake mtu atajaye jina la Bwana bure kwa kusudi la kuficha uongo na unafiki!

Watu siku hizi hawaaminiani wao kwa wao kwa sababu wenyewe hawasemi yaliyo kweli hata wanapoapa katika jina la Bwana. Jesu anatukatalia kata kata tusiape. „Maneno yenu yawe Ndiyo,ndiyo; Siyo,siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu.“ (Mathayo5:37) Ikiwa tunaapa na kusema uongo, hatusemi uongo tu kwa watu, bali pia kwake Mungu mwenyewe. Kiapo kisicho sawa kinahesabiwa chini ya Amri ya Tatu, inayotuonya tusiseme ovyo dhidi ya jina la Bwana. Ndiyo maana Biblia latuambia, „Kicho mbele ya Bwana ndiyo mwanzo wa hekima.“ Sisi sote twahitaji sana kicho mbele ya Bwana tusije tukaanguka katika dhambi.

Mungu humchukia sana mtu amjuaye na hata hivyo anaacha kumwita wakati wa shida au kutazamia jibu au uongozi wake, lakini badala yake anaenda moja kwa moja kwa mpiga ramli atumiaye jina la Bwana bure na ndipo kudai uwezo wa kufunua yaliyopita, yaliyopo au yatakayokuja (Kumbukumbu la Torati 18:9) Tena Mungu asema, „Na mtu yule atakayewaendea wenye pepo, na wachawi, ili kuzini pamoja nao, nitakaza uso wangu juu ya mtu yule, nitaamtenga na watu wake.“ (Mambo ya Walawi 20:6) Pia inakatazwa kujenga uhusiano na wafu na kupokea ujumbe kutoka kwao. Dhambi za namna hiyo bila mjadala yamtenga mtu na Mungu na kufungua moyo wake kwa shetani na roho zake. Aonavyo Mungu, ukafiri ya namna hii ni sawa na uzinzi. Hilo ni ya kuchukia sawa na mtu asiye mwaminifu kwa mke wake na kutumia hata fedha ya mkewe na kwenda kwa malaya. Basi haishangazikwamba Bwana anaita mambo hayo kuwa „umalaya wa kiroho“(Mambo ya Walawi 20:6) na kuwasema watu kama hao „ni kizazi kiovu na yenye uzinzi.“

Bara Afrika na Asia watu hubeba hirizi, ili kujilinda na mabaya. Huwa wanatoa pesa nyingi kujipatia vitu hivi ndipo kuvitegemea kabisa. Pia wanaandika “barua za kuloga” ili kufaulu zaidi katika biashara au kwa kuomba mapenzi kati ya watu wawili. Mataifa yanaoendeleza desturi za ushirikina, kwa kweli hawamjui Mungu. Katika nchi kadhaa wanaonyesha hata matendo ya uramali, uchawi na ulozi ndani ya television. – Sisi kama Wakristo tunahesabu maonyesho kama hayo pamoja na mafundisho yake kuwa mashambulio ya kishetani yanayolenga waangalizi wasiotofautisha mema na mabaya. Matokeo yake mabaya ni kama kufungua malango ya kuzimu. - Basi Bwana hutuonya waziwazi dhidi hatari hizo zote, kwa sababu ni wazi kabisa jinsi anavyotutenganisha na Yeye. Bwana Yesu tu aweza kuwaweka huru na mapingu hayo watu wa namna hii. Kusoma falaki, kwenye mkono na kuangama kwa ajili ya kusihi roho za wafu kutokea ndiyo njia fupi za kuelekea kuzimuni. Wako wanaoeleza matokeo ya mbeleni katika hoteli nyingi kule India wakiwangojea wageni na kuwasomea matokeo yao ya mbeleni. Pia wanachora picha ya macho yaliyochomwa na mkuki ili kukinga jicho baya. Wengine huning’inisha hirizi ndani ya gari, vyuma vya farasi kwenye farasi zao na kuguso mbao kwa ajili ya kukinga msiba mkubwa. Watendao hayo huamini zaidi katika nguvu za giza kuliko katika ulinzi wa Mungu, Baba yao wa mbinguni. Wamo ndani ya mapingu ya giza za dunia hii ka ajili ya vitendo vya aina hii.


05.9 - Kumkufuru Mungu

Watu fulani wanaenda mbali mno katika kutamka jina la Mungu wanapoapa kwa kusudi kwa Mungu na Kristo yako. Wanajipanga wenyewe pamoja na wale wanaoasi dhidi ya jina la Baba, la Mwana na la Roho Mtakatifu. Shetani ndiye adui wa awali wa Mungu. Kumkufuru Mungu ndiyo namna ya kuelekea kwa pepo mbaya wanaoruka kama uchafu toka kuzimuni. Ikiwa fulani anatakiwa kusoma barua ndefu, ambamo ndani yake jina la Kristo linalaaniwa, kwa vyovyote atanusa harufu ya kuzimu usoni mwake. Kitabu cha Mambo ya Walawi 24:14-16 twasoma, “Mtoe huyu aliyeapiza nje ya marago; na wale wote waliomsikia na waweke mikono yao kichwani mwake, kasha mkutano wote na wamwue kwa kumpiga kwa mawe. Nawe nena na wana wa Israeli na kuwaambia, Mtu awaye yote atakayemlaani Mungu wake atachukua dhambi yake. Naye atakayelikufuru jina la Bwana hakika atauawa; mkutano wote watamwua kwa kumpiga kwa mawe; kama ni mgeni, kama ni mzaliwa, hapo atakapolikufuru jina la Bwana atauawa.”

Twahitaji kuwa wanyenyekevu na waangalifu tunapomsema au kumhukumu mwenye kufukuru. Watu wengi waliopagawa na mapepo walikuwa vipofu kwamba, walipofikiri kumtumikia Mungu, kwa kweli walikuwa wanapigana na Yeye na Masihi wake (Yohana 15:19-21 na 16:1-3). Viongozi wa cha Mungu na wenye hekima ndiyo wale waliomhukumuYesu afe, wakidai kwamba amemkufuru Mungu. Ingawa walikuwa ni viongozi wa kiroho wa Waisraeli, hawakutambua kwamba Yesu alikuwa ni Mwana pekee wa Mungu aliye hai. Katika shauku yao kwa ajili ya Mungu, wao wenyewe wakamkufuru Masihi yake aliyetiwa mafuta kwa kumweka wakfu. Wakamtemea mate usoni na kumpiga kichwaniViongozi wa wale watu wazamani walishindwa kutambua au kumkubali Bwana wao aliyekuwa hapo kati yao. Badala yake, wakamkataa na kumsulibisha. Twasema kwa huzuni kwamba, hata siku hizi karibu wote wao bado wanamkataa Yeye.

Kama hao wana wa Yakobo, Waislamu wanafikiri kwamba wanamkufuru Mungu, ikiwa wataamini katika uungu wa Kristo na kwamba alisulibiwa. Wao nao walirithi kichukizi ya Wayahudi, ambacho hakiwezi kusahihishwa, na hivyo kupiga vita imani ndani ya Utatu wa Mungu. Wanakaribisha chuki pasipo hurumakwa ajili ya Mwana wa Mungu aliyesulibishwa. Lakini hivyo wanafunua na kuonyesha hali ya kukufuru dhidi ya Mungu Baba, Mwana na Roho Mtakatifu kwa njia ya chuki yao kwa ajili ya kanunu ya Utatu. Basi, upande wa pili, dini ya Uhindi inkataa mamlaka ya pekee ya Kristo, wakimhesabu kuwa mungu mmoja kati ya wengi.

Baadhi ya Wakristo wanaorudi nyuma wanasukuma ukafiri wao mbali mno hata kwa kumwabudu Shetani. Wakati wa ibada zao wanaendeleza karamu za ovyo na hata kutoa sadaka ya damu kwa Shetani. Wanageuza vibaya na kuiga Sala ya Bwana kwa maneno ya kubadili maana yake wakimwabudu Shetani. Hii ndiyo jinsi nguvu ya giza inapomfikia kila mtu anayekataa kwa kusudi wokovu wa Mungu ndani ya Kristo.

Lakini ndani ya Kristo kuna ukimbilio ambapo jehanum haiwezi kuingilia. Mchungaji wetu mwema asema, “Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua , nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu. Mimi na Baba tu umoja” (Yohana 10:27-30).

Wayahudi walitaka kushika Amri ya Tatu kwa karibu kabisa, hata wakaogopa kutamka jina kuu la Mungu kwa kukosa , au hata kwa kukosea tu. Sote twafahamu kwamba jina la kiebrania ya herufi nne tu kwa ajili ya Mungu ni YHWH. Kwa sababu ya hadhi takatifu ya jina hilo, tangu mwaka 300 hivi kabla ya kuzaliwa kwake Yesu (BC), Wayahudi walianza kujizuia kulitamka walipokuwa wakisoma Maandiko, na wakatumia jina “Adonia”. “Yehova”ndilo neno lililotungwa na watukutokana na kuunganisha vokali za neno “Adonia” ndani ya konsonanti za “YHWH”. Ikatumika hivyo hadi mwaka 1520 AD. Jina la awali ya mungu na kutamkwa kwake inafikiriwa kuwa “Yahweh”.

Jambo hila pengine litatupeleka kwa swali hilo: Je, tutamke jina la Mungu kwa vyo vyote? Basi namna gani tungetamka jina la Mungu, ili tusije tukahukumiwa ?


05.10 - Kutamka jina la Mungu sawa

Kwa vyo vyote Amri ya Tatu haitukatazi kutamka jina la Mungu katika roho ya kweli. Hapo kuna ahadi kuu, “Hutamki jina la Bwana bure unapolitumia katika imani, upendo na shukrani.” Bwana atatumia ushuhuda wa imani yako kama mfereji wa msamaha au upatanisho uwe uamsho katika maisha ya rafiki zako. Jina lake halina nguvu ya mwujiza, ambalo tungeweza kutumia kufuatana na mapenziyetu au kutaka kwetu. Bwana mwenye uzima atatenda kwa njia ya jina lake kufuatana na kuona kwake mbele na mpango wake. Mtume Petro alimwambia yule mtu mwenye kupooza, “Kwa jina la Yesu wa Nazareti, inuka na kutembea. Baadaye akathibitisha kwa wazee na viongozi wa watu, “Kwa jina la Yesu Kristo wa nazareti mtu huyu anasimama mzima hapo mbele zenu” (Matendo ya Mitume 3:6, 16 na 4:10). Ufahamu wetu wa jina la Yesu na uwezo wake tungeipa kina zaidi. Mwanatheologia mwenye sifa, Schlatter, alikuwa amejifunza maandiko yote ya kiyunani ya Agano Jipya kimoyo, lakini mwisho wa maisha yake aliandika kitabu kiitwacho, “Je, tunamfahamu Yesu ?” Basi tusingesema kwa juu juu habari ya Yesu, badala yake tungmfahamu zaidi na zaidi Bwana wetu. Tungkua kwa kina ndani ya Neno lake kwa kusali. Tungetafakari juu ya kila neno, ndipo kwa vyo vyote Mungu atasema nasi kwa njia ya Neno lake, ikiwa limeshika mizizi kwa chini ndani ya mioyo yetu.

Itatusaidia sana kuwa mashahidi bora kwa Yesu, ikiwa tutajifunza kimoyo sura nzima au mistari mingi kutoka kwa Agano la Kale na Jipya, kwa sababu Neno la Mungu ni nguvu, nalo latupatia hekima ya Roho Mtakatifu. Abarikiwe mwanaume au mwanamke aijazaye kumbukumbu yake ya ndani kwa Neno la Mungu. Zaidi ya hapo, ushuhuda za waumini na historia za watu wa Mungu waliokomaa, zaweza kutuchochea katika ufahamu wetu wa jina la Mungu na kazi zake zaidi, na hivyo tutaimarika kiimani. Tunakuwa na furaha tunapozingatia kwa taratibu ya kila siku juu ya Neno la Mungu, na hata rafiki zetu watafurahi kwa njia ya ushuhuda wa imani yetu.

Tunaposikiliza Neno la Mungu, hatuwi peke yetu tena, bali tunaendelea kumfahamu Bwana wetu zaidi na zaidi. Tunaweza kumwita kwa sala moja kwa moja, kwa sababu twafahamu jina lake. Anasema nasi kwa neno la Biblia nasi tunamjibu katika maombi yetu. Kweli tumependelewa sana kwa sababu ya kuweza kusema na Mwumbaji wetu habari ya kila dhambi, ugonjwa, matatizo au hata mateso fulani, naye anatusikiliza ! Mausia yake ni bora kuliko ya daktari au ya mtalaamu wa kuchunguza roho zetu (saikologisti). Mungu atupenda zaidi ya baba yetu wa hapa duniani. Anatusamehe dhambi zetu kabisa kwa sababu ya kifo cha kulipia cha Yesu, naye anatujalia nguvu ya kurithi uzima wa milele kwa njia ya Roho Mtakatifu aishiye ndani yetu.


05.11 - Tumshukuru Mungu kwa mioyo na nia zetu !

Je, tuko tunamtukuza Mungu kweli na kumshukuru kwa moyo wa dhati? Tukumbuke basi, kwamba Mungu Mwenyezi ndiye Baba yetu, Mwanawe wa pekee ndiye Mkombozi wetu na Roho Mtakatifu ndiye Mfariji wetu wa daima na nguvu yetu, na kwa yote hayo tuendelee kuwa na shukrani. Badala ya kumwabudu Mungu kwa kutetemeka na hofu, tungemwabudu Yeye kama watoto wake wanaofurahia kazi Yake kwa ajili ya baraka ya tumaini letu na ukombozi ulio kamili; hatutakiwi kuendelea kuwa wafu kwa ajili ya dhambi tena, lakini wenye uhai daima ndani yake Kristo. Hivyo, usipoweza kuimba sifa ndani ya kwaya, bado unaweza kuimba wewe peke yako; na kama huwezi kuimba na midomo yako mwenyewe, utaweza kuimba moyoni mwako. Kama yeyote atatamka jina la Baba , na ya Mwana nay a Roho Mtakatifu kwa ushujaa, katika sala au shukrani ya furaha, basi wanamheshimu Mungu Mwenyezi na kumpendeza kwa ajili ya kumtukuza.

Kama yuko mtu asiyemfahamu MUngu, au kama moyo wake umekuwa mgumu, au dhamiri yake inashitakiwa kwa sababu ya dhambi zilizofichika, basi anatakiwa kupokea mwongozo wa Mtume Petro anaposema: “Na itakuwa kila atakayeliitia jina la Bwana ataokolewa” (Matendo ya Mitume 2:21). Twarudia kusema, tumependelewa kuweza kusema moja kwa moja na Mungu, Baba yetu, kwa njia ya jina la Yesu, naye atatujibu. Tunaweza kumkaribia Mungu kwa sababu Yeye ametukaribia kwanza. Jina la Mungu, “Baba yetu”, latuhakikishia kwamba, baraka zote za mbinguni zimeandaliwa kwa ajili yetu. Jina la Yesu hutingisha misingi ya jehanum, kwa sababu alishinda dhambi, kifo na shetani. Roho Mtakatifu humtukuza Mwana wa Mungu, kwa sababu katika jina lake anatupatia uzima wa milele na nguvu ya pekee ya Mu ngu. Pia anatujalia usalama, usafi, furaha na Amani. Jinsi jua linavyoleta miali yake isiyoweza kuhesabika hapo duniani siku kwa siku, ndivyo majina ya Mungu wetu wa Utatu anavyotujalia neema juu ya neema. Nani saiyetaka kutoa shukrani kwake Baba au sifa kwa Mwana, na kusali katika nguvu ya Roho Mtakatifu? Ujifunue wazi kwa Roho ya kutuliza wa Bwana wako, ndipo utajifunza jinsi Mungu kweli anavyojibu maombi yako. Toa sifa zako katika jina la Yesu, maana ndivyo inavyokubalika na Baba yako. Umshukuru na kumtukuza Yeye, kwa sababu anakupenda, amekukomboa na kukujalia uzima wa milele.


05.12 - Ushuhuda wetu wa Imani mbele ya wengine

Nani ataweza kunyamaza wakati moyo wake unafurika na shukrani na sifa ? Na nani ataweza kutunza hali ya kupokea wokovu ndani yake kama siri, anapofahamu kwamba Mungu anataka watu wote wapate kuokolewa? Kazi ya kuwafikia waliopotea sio chaguo letu tu, lakini Bwana Yesu mwenyewe anatuagiza twende na kueleza Habari Njema kwa yeyote. Ushindi wa Yesu Kristo na ukuu wake lazima litangazwe. Mtume Petro anatusihi, “Mwe tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu“ (1.Petro 3:15). Yesu mwenyewe naye atuonya, „Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni. Bali mtu yeyote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni“ (Mathayo 10:32-33).

Wakati Mtume Paulo alipokuwa akitaabishwa na magombezi ya adui za Mungu, Bwana alimtokea usiku na kumfariji: „Usiogope, bali nena, wala usinyamaze, kwa kuwa mimi ni pamoja nawe, wala hapana mtu atakayekushambulia ili kukudhuru; kwa maana mimi nina watu wengi katika mji huu“ (Matendo ya Mitume 18:9-10). Tena akamhakikishia, „Nitakuokoa na watu wako Wayahudi, na watu wa Mataifa, ambao nakutuma kwao, uwafumbue macho yao, na kuwageuza waiache giza na kuielekea nuru, waziache na nguvu za Shetani na kumwelekea Mungu; kisha wapate msamaha wa dhambi zao na uridhi miongoni mwao waliotakaswa kwa imani iliyo kwangu mimi“ (Matendo ya Mitume26:17-19).

Jioni ile ya ufufuo wake, Yesu aliwajalia wanafunzi wake walioogopeshwa mamlaka yake tukufu, iwapo walikuwa wamefunga kabisa milango yao, „Jinsi Baba anavyonituma mimi, mimi nami nawatuma ninyi.“ Baada ya kujifunua hivyo kwao, aliwavuvia na kuwaambia, „Pokeeni Roho Mtakatifu. Wo wote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa“(Yohana 20:21-23). Unapojifunza kabisa maneno hayo na kuyatafakari moyoni mwako, utapokea nguvu na uongozi kwa ajili ya kufanya uinjilisti kwa njia uliyo bora, ili kuwafikia wasioamini na kukataa, na pia kwa wapagani waliopotea hadi sasa.


05.13 - Kutumika katika Jina la Bwana

Bwana anaposema nasi kupitia Neno Lake nasi tunapoitika kwake katika sala na shukrani na kukiri jina lake takatifu mbele za marafiki na pia kwa adui, basi ndipo tutagundua enzi ya jina lake. Katika hilo jina lake Mitume waliwaponya wagonjwa, wakatoa mapepo wachafu na kuwafufua wafu. Yesu mwenyewe alituliza bahari iliyochafuka kwa neno lake. Yeye pia aliongeza mikate mitano kwa ajili ya kushibisha maelfu. Alisamehe makosa ya watenda mabaya waliotubu akawabariki na uzima wake wa milele. Yesu akatamka, „Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi“(Yohana 5:17). Si kwamba sisi tunasema tu katika jina lake, lakini Yeye naye hutenda kazi kupitia udhaifu wetu. Wakati wo wote Baba, Mwana na Roho Mtakatifu wanatawala ndani ya moyo wa mwumini, Mungu anatenda miujiza kwa njia ya maisha yake. Si kitu kwake kama watoto wake ni wadogo sana, maana ni Baba mwenyewe anayekamilisha kazi wanayoifanya.

Ushuhuda wote wa ukweli na wa kufaulu unatoka kwenye asili ya ushuhuda wa maisha ya waumini: Twaweza kumbariki Mungu na wakati uo huo kutokumtii. Roho Mtakatifu tu atuongoza kuendesha maisha yetu yawe takatifu na kututakasa kwa sababu Yeye mwenyewe ni takatifu. Yesu alitufundisha kuomba maneno ya kwanza katika Sala ya Bwana, kutakasa au kutukuza jina la Bwana kwa midomo yetu na maisha yetu. Sala zetu zingekuwa uongo, na pia ushuhuda wetu, kama maisha yetu yangekataa enzi ya Mungu na kutokuonyesha unyenyekevu wa kweli.

Hakika, tunatenda dhambi kinyume cha kutaka kwetu, lakini tunajisikia kuvunjika mbele yake Mtakatifu. Dhambi zetu siyo jambo la sikuzote machoni pa Mungu, na inatupasa kukumbuka daima kwamba kunamhuzunisha na matendo yetu mabaya. Lakini Roho Mtakatifu hutawala ndani ya kila mtu atubuye na kumfariji, tena amhakikishia kwamba damu ya Yesu anamsafisha na dhambi zote (1.Yohana 1:19). Neno la Baba nalo latutia moyo tuwe na imani na tuishi katika jina la Mungu wa Utatu. Tutaendelea kugundua utakaso wetu kwa uwezo ua upendo wake wa kuvumilia na wa kushinda yote.

Je, unafahamu kwa kweli na kutambua jina lake Mungu? Jina lake takatifu limo kwenye ulimi wako? Je, Roho wa Bwana kweli anatawala ndani ya moyo wako? Kama ni hivyo kweli, ndipo tu utaweza kutamka jina la Baba, la Mwana na la Roho Mtakatifu kwa namna ilivyo sawa kwa kicho na upendo. Haya, Bwana na akulinde na hali ya kutamka Jina lake ovyo, na akuongoze umsifu kwa furaha na shangwe maisha yako yote.

www.Waters-of-Life.net

Page last modified on August 01, 2017, at 01:58 PM | powered by PmWiki (pmwiki-2.3.3)