Waters of Life

Biblical Studies in Multiple Languages

Search in "Kiswahili":
Home -- Kiswahili -- The Ten Commandments -- 09 -- Seventh Commandment: Do Not Commit Adultery
This page in: -- Afrikaans -- Arabic -- Armenian -- Azeri -- Baoule? -- Bengali -- Bulgarian -- Cebuano -- Chinese -- English -- Farsi? -- Finnish? -- French -- German -- Gujarati -- Hebrew -- Hindi -- Hungarian? -- Indonesian -- KISWAHILI -- Malayalam? -- Norwegian -- Polish -- Russian -- Serbian -- Spanish -- Tamil -- Turkish -- Twi -- Ukrainian? -- Urdu? -- Uzbek -- Yiddish -- Yoruba?

Previous Lesson -- Next Lesson

TOPIC 6: AMRI KUMI - Kuta za ulinzi wa Mungu zinazolinda wanadamu wasianguke
An Exposition of the Ten Commandments in Exodus 20 in the Light of the Gospel

09 - Amri Ya Saba: Usizini



KUTOKA 20:14
“Usizini”


09.1 - Kawaida maalum (Institution) na kusudi kuu la ndoa

Mungu alimwumba mtu kwa mfano wake; kwa mfano wa Mungu alimwumba. Aliwaumba mwanaume na mwanmke. Aliwateua wote wawili warudishe kama kioo mfano wake. Wote wawili wakiwa na usawa wa kiroho. Uhusiano wa mwanaume na mwanamke kwake Mungu ndiyo siri ya ustahi na heshima yao.

Mungu alimwumba mwanamke mmoja kwa ajili ya mwanaume mmoja. Angalia kwamba, hakuwaumba wawili, watatu au wanne kwa ajili yake. Mungu ndiye nafsi ya tatu ndani ya agano la ndoa iliyo sawa. Anawahakikishia washiriki wote wawili wawe na tabia moja, lengo moja, na akiwasahihisha wote wawili na kuwafanya kuwa na umoja wa kiroho. Anawaongoza waishi maisha ya kujitoa kama sadaka, ambamo ndani yake upendo Wake ndiyo kiungo cha ukamilifu. Mtu ampendaye Mungu anaweza kumpenda mwenzake wa maisha bila kukoma. Bwana katika rehema zake, huwaunganisha watu wawili wa hali ya kujipendeza, akikusudia kwamba, wote wawili watashinda hali hiyo ya kujipendeza binafsi kwa nguvu ya upole wake.

Mungu alimwumba mwanamke kutoka kwa mwanaume, wala si kwa kubadilisha. Rabi fulani wa Kiyahudi anaeleza kwamba, Mungu hakuchukua ule mfupa wa ubavu kutoka kwenye kichwa cha mwanaume, isiwe mwanamke awe na mamlaka juu yake; wala hakuichukua kutoka katika mguu wa mwanaume, asije akamkanyage mkewe. Aliuchukua katika ubavu wake, ili mke asimame sambamba naye, amsaidie, amkamilishe na ashiriki masumbufu yake.

Kabla ya mtu kuanguka katika dhambi, jina la mke lilikuwa „isha“, namna ya kike kwa kiebrania wa neno la „ish“, ambalo ni mume. Herufi ya „a“ mwisho wa neno inaonyesha kwamba, neno ni la kike kwa kishemu na hutokea katika kiarabu na kiebrania. Mke alihusika kwa usawa kwa mume wake katika mambo yote na haki zake zote. Hivyo si ajabu kwamba, mwanaume atawaacha baba na mama, alivyosema Mungu, na ataambatana na mkewe, wala si kwa kubadilisha. Wazazi kadhaa wangeungama na kumruhusu mume mwenye umri mdogo aachane na familia yake kwa shabaha ya kuishi na amani pamoja na mke wake. Hao wawili wanatakiwa kuunda familia iliyo huru kabisa na kuendeleza maisha yao pamoja mbele za Mungu, wakiunda umoja imara wa roho, moyo na mwili. Upendo wa kutwaana kimwili na tamaa ni vipawa vyema toka kwa Mungu, ili kuendeleza uhusiano ya ndoa ya heshima kwa tegemeo la kupata watoto kwa neema ya Mungu. Kwa vyovyote Mungu hakueleza upendo wa kimwili ndani ya ndoa kuwa chafu au najisi, lakini kuwa ya baraka na takatifu kwa muda wote mwanadamu anavyoishi mbele za Mungu na kuwa mwaminifu kwa mwenzake.


09.2 - Udumu wa Ndoa

Ndoa iliharibiwa mara washiriki wote wawili walipoachana mbali na ushirikiano wao na Mungu. Kuanguka kwa Mwanadamu ndani ya dhambi ilianza ndani ya roho na moyo wake mwenyewe, wala si ndani ya mwili wake. Mwanadamu aliambukizwa na kiburi cha yule mwovu. Mwanamke na mwanaume walitamani kuwa sawa na Mungu. Jaribu hilo lilianza ndani ya roho wa binadamu na katika kutaka kwake na ilitokeza adhabu ile kuu iliyoharibu maeleano yote ya maisha. Mwanamke akawa chini ya mwanaume na alishindwa kuelewa namna ya kuendeleza maisha duniani peke yake. Pia ilimpasa mwanamke kuzaa watoto akipatwa na maumivu mengi, wakati mwanaume alitakiwa kuchapa kazi sana kwenye shamba la miiba na kwa hali ngumu. Tangu hapo pia kufa kukawa ni mshahara wa dhambi.

Kuanguka kwa mwanadamu ndani ya dhambi ilidhuru pia ndoa kwa vibaya sana; hata hivyo ndoa ya watu wawili iliendelea kuwapo hata baada ya uuasi wa binadamu dhidi ya Mungu. Kwa bahati mbaya watu wakati wa Agano la Kale walianza kuchukua wake zaidi ya mmoja, iliyowapatia shida za hatari. Pia walileta taabu kubwa juu ya watoto wao kwa njia ya kutokumtii Mungu katika namna ya mke mmoja wa ndoa. Ndani ya Ishmaeli, mzaliwa wa kwanza wa Ibrahimu, ambaye Uislamu unamtambua kuwa baba wa Waarabu na Waislamu wote, tunaona mfano maalum wa taabu kudumishwa kutokana na tendo la kutokutii kwa Ibrahimu, aliyekuwa mtu wa Mungu. Siyo siri kwamba, vita zinazoendelea katika vizazi vya ndugu wawili wa baba mmoja, Ishmaeli na Isaka, zinatingisha mataifa ya Mashariki ya Kati hadi siku ya leo.

Yakobo akawa na watoto kutoka kwa mkewe Raheli, mpenzi wake; pia na toka kwa Lea, mkewe wa kwanza, na baadaye pia wengine toka kwa wanawake wa kinyumba. Mfalme Daudi akapata kuwa mwuaji baada ya kufanya mapenzi na mwanamke mwenye ndoa, lakini alitubu kwelikweli. Wengi wanatenda dhambi kama Daudi, lakini wachache wanatubu kama yeye! Sisi sote tungejifunza kwa moyo Zaburi ya 51 na kufuata ungamo wa kweli wa huyu mtu wa Mungu. Sulemani mwenye hekima kuu baadaye alitenda kipumbavu na bila hekima alipowaoa mamia ya wanawake wa kipagani na kuwaruhusu kuingiza hata miungu yao migeni ndani ya taifa lake. Sanamu hizo ziliwafanya watu wake kurudi nyuma na kuachana na Mungu mwaminifu.

Hali ya kuwa na wake zaidi ya mmoja haijafutwa hadi leo kwa Waisraeli. Wayahudi wanaohamia kutoka katika nchi za kiarabu wanaweza kuendelea na wake zao wote. Pia kuachana na kuoa tena ni halali, ikiwa mke wa kwanza hakujaliwa wana.

Ingawa Mungu alivumilia hali ya wake zaidi ya mmoja kwa enzi za Agano la Kale na hivyo kuwaachilia wavunja wa taratibu za ndoa wateseke na matokeo ya dhambi zao, aliamuru wazinzi wa kiume na wa kike wapigwe kwa mawe wafe (Mambo ya Walawi 20: 10-16 na Kumbumumbu la Torati 22:22-26). Twashindwa kusoma bila kutetemeka ile orodha ya maadhibu ndani ya amri za Musa kwa ajili ya namna mbalimbali za uzinzi zinazotendeka hata leo, kwa binafsi na hata hadharani. Hata ndani za familia kadhaa na katika mashirika namna za kutwaana zinatendeka, ambazo zingepasa kuwashukia wale washiriki adhabu ya kufa. Hakuna ruhusa yoyote katika Biblia ya kutwaana waume kwa waume; tendo hilo pia iliadhibiwa kwa kufa. Ya kuchukiza kuliko yote hayo kwa Mungu ni wanaume au wanawake kutwaana na wanyama. Hakuna namna yoyote ya kutwaana kimwili inayoruhusiwa na Mungu ila ndani ya ulinzi wa ndoa kati ya mume na mke wake. Yeyote anayepinga taratibu hiyo iliyowekwa na Mungu atakuwa chini ya laana na mapatilizo ya Mungu. Wakati wowote ulimwengu unahitaji ungamo wa kweli na kuendelea, pia na usafi wa akili, moyo na utendaji.


09.3 - Mateso kutokana na uasherati

Kwa kawaida uasherati hauanzi na mshiriki mmoja wa ndoa kutwaana na mtu mwingine, lakini inatanguliwa na tabia ya kuachana na Mungu polepole, na tokeo lake ni kwamba, mwenzake wa ndoa naye ataingia katika tabia iyo hiyo. Lakini yeyote atakayefaulu kuendelea katika uhusiano wa karibu na Mungu, huyu ataendeleza upendo imara zaidi na ya kukomaa kwa ajili ya mwenzake wa ndoa, naye hatatenda uasherati kwa hali yoyote ile. Ndiyo maana kwamba, kawaida uasherati unatanguliwa na mshuko na uharibifu wa ushirikiano kiroho, kwa kujisikia, na baadaye matendo yote pia. Ndipo mume na mke hawawezi kueleana tena na kuzama zaidi na zaidi ndani ya matope ya dhambi.

Kuacha uaminifu wa ndoa karibu kila mara kunaanza ndani ya akili. Akili inaona sura za kupendeza ambazo, zisipong’olewa kabisa na kukataliwa katika jina la Yesu, zitatatanisha na kamata ndani ya mtandao mwenye hatari ya kuua. Mwishoni mtu hutafuta namna ya kuzifanyia kazi hizo ndoto chafu, ndipo kwa kukusudia atatenda dhambi. Pengine mtu yule mwingine ni wa kupendeza na kumvuta aelekee dhambini, hadi wote wawili wataingia majaribuni hata bila nguvu ya kujizuia. Labda dhamiri itaamka mwanzoni, lakini uasi huo inapoongezeka, moyo utaendelea kuwa ngumu, ndipo uasherati haitakuwa ni uzoefu tu lakini itakuwa hali ya lazima. Hata hivyo, tangu mwanzo wa kuendeleza tabia hiyo ya dhambi, huyu mzinzi anafahamu kwamba kazi yake ni chafu na sio ya halali. Yeye aanzaye kutenda dhambi baadaye itampasa aendelee kuitenda.

Dhambi inapata kuwa nguvu ya kuendesha tabia hiyo ndani yake ajifunguaye kwa jambo hilo; lakini Bwana asifiwe, bado kuna tumaini la kudumu milele ya kuweze kuwekwa huru na dhambi. Yesu asema, „Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi ….. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli“ (Yohana 8:34-36). Neema na Roho wa Bwana Yesu Kristo zaweza kufikia maeneo ya ndani kabisa ya dhamiri ya binadamu, nazo zaweza kutakasa na kutuponya kabisa. Makovu kadhaa na majaribu fulani zitasalia, lakini damu ya Yesu Kristo hutusafisha na dhambi zote na kututia nguvu kushinda hayo majaribu. Kama Mwana wa Mungu atamweka huru mtu, atakuwa huru kweli.


09.4 - Ndoa inayoendelezwa na Yesu

Yesu alithibitisha ndoa ya mume na mke mmoja, naye akakazia kwamba, umoja wa mume na mke ni ushirikiano wa kudumu maisha yote (Mathayo 19:4-6). Aliwajibu wale walioshindana naye akisema, „Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke; akasema: Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja?“ Hivyo basi, hao sio wawili bali mwili mmoja. Kwa hiyo Mungu alichounga pamoja, mwanadamu asikitenganishe (tazama pia Marko 10:1-12).

Kwa mistari hii Yesu amethibitisha namna ya utatu inayotengenezwa kati ya Mungu, mume na mke, ambao ameupiga muhuri na Roho Mtakatifu ndani ya mioyo ya wafuasi wake. Yeye anatakasa roho zetu, moyo na mwili, ndipo anaturuhusu tuwe hekalu la Mungu aliye hai na kuendeleza maisha ya ndoa kuwa kama paradiso ndogo, ambamo ndani yake Bwana anaishi na kutawala. Msamaha wa dhambi kwa damu ya Yesu unatupatia moyo mpya na mwili uliotakaswa naye anaumba malimwengu mapya katika familia nzima. Ndani ya Kristo maisha ya ndoa inapokea maana mpya, hali ya baraka, na pia inapatia ndoa kusudi mpya. Taratibu ya thamani kuu ni kwamba, Mkristo asimwoe mtu asiyeamini. Njia hii inazuia matatizo mengi. Kumpenda Yesu ina maana ya kumpenda mwenzako wa maisha vilevile na kumhudumia kwa uaminifu hadi kufa.

Si Yesu wala si mitume wake walioondoa shauku ya mwanaume na upendano wake kwa mke wake. Pia hawakufuta utii wa mwanamke upande wa mwanaume. Hata hivyo Roho Mtakatifu huwaongoza watu wa ndoa kuwa na uvumilivu na upole katika maeneo yote ya maisha. Mtume Paulo alimwagiza kila mume kumpenda mke wake jinsi Yesu alivyojitoa kama sadaka kwa ajili ya kanisa lake. Upendo wa kweli si kutimiza tamaa tu bila kujizuia, bali ni kumhudumia mwenzake wa maisha kwa heshima wao kwa wao. Kujitawala kunatokana na kudumu ndani ya uongozi wa Roho Mtakatifu, ndipo ndoa haitakuwa mahali tu pa kutwaana kwa mapenzi, lakini ndoa ya kuhudumiana inayomtukuza Mungu.


09.5 - Ndoa katika Agano Jipya

Yesu aliweka kanuni ya juu kwa ajili ya roho zetu, moyo na mwili. Alisema, „Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake“ (Mathayo 5:28). Kwa kanuni hiyo wanaume wote wanaonekana kuwa wenye dhambi mbele za Mungu Mtakatifu. Tunahitaji kukiri dhambi zetu kwake Mungu wazi, maana hakuna aliye msafi mbele za Mungu. Tunatakiwa kuungama dhambi zetu za nyege kabisa, ili tuwe na msingi kwa ajili ya utakaso ndani ya shule ya Yesu. Wote tunahitaji hali ya kuvunjika mioyo mbele za mhukumu wa milele, ambaye yeye wakati uo huo ni Mwana Kondoo wa Mungu mnyenyekevu aliyepeleka mbali dhambi za ulimwengu wote. Yeyote amwelekeaye yeye atapewa haki, hali amesafishwa na kutakaswa wakati wowote, ambao bado ni muda na nafasi ya wokovu.

Wakati wazee wa taifa la Wayahudi walipomleta mwanamke aliyefumaniwa katika tendo la uasherati mbele za Yesu, yeye hakupuuza dhambi yake, lakini baada ya kuwapa hao wazee kutafakari habari zao wenyewe, aliwataka wampige kwa mawe kufuatana na agizo la amri. Lakini aliweka sharti ndogo akisema: Yule ambaye hajatenda dhambi awe wa kwanza wa kumtupia jiwe. Basi hapo wote walichomwa na kushitakiwa ndani ya dhamiri zao. Kati yao walikuwapo makuhani wakuu, wazee na mitume wa Kristo mwenyewe. Wote waliondoka polepole, mmoja baada ya mmoja. Mwishowe Yesu na yule mwanamke mzinzi walibakia peke yao. Hapo basi Yesu angemtupia jiwe la kwanza, maana yeye alikuwa ni mtu pekee bila dhambi aliyebakia. Lakini yeye hakumpiga kwa mawe. Alimwambia arudi nyumbani kwake wala asitende dhambi tena. Je, Yesu alivunja amri kwa kutokumpiga kwa mawe? Hapana! Bali alijitwisha dhambi yake mwenyewe akafa badala yake. Hivyo alikuwa na haki kumsamehe dhami yake. Kifo cha Yesu msalabani tu kinawaweka huru wazinzi kutoka katika hukumu chungu. Kila mtu atendaye uasherati katika mawazo, maneno au matendo akitubu, atakuta wokovu kipekee ndani ya Yesu huyu aliyesulibiwa.

Yesu alikataza kuachana na kuthibitisha kudumu kwa umoja wa watu wawili waliofunga ndoa hadi kufa. Yeyote anayefikiria habari ya kufunga ndoa anahitaji kuomba kwa makini kuhusu hatua hiyo. Mwanaume anatakiwa kuuliza, „Huyu ndiye aliyetayarishwa na Mungu kwa ajili yangu, au mimi namchagua tu kutokana na nia ya umimi? Tunapatana kwa habari ya umri, tabia, vipawa, elimu na familia (ukoo wake na wa kwangu)? Je, yule mtu ninayemfikiria anasimama imara ndani ya imani juu ya Bwana wa utatu, au anayo uhusiano wa kimawazo tu juu ya Mungu? Maswali kama hayo na mengineyo yanatakiwa kuulizwa na kwa maombi kufikiriwa kabla ya kukata shauri ya kufunga ndoa, wakati ambapo bado kuna nafasi ya kuamua. Kuvunja uchumba ni bora kuliko kuingia katika agano la ndoa wakati hao wawili hawapatani vema.

Kutwaana kimwili kabla ya kufunga ndoa ingezuiliwa kwa gharama yoyote ile. Ukimpenda kweli mchumba wako utamheshimu na kutokumchafua au kuvunja sifa yake. Hakuna awezaye kuwa na hakika kwamba ataendelea kuwa hai hadi siku ya arusi. Basi, wewe kama mwanaume kijana unatakiwa kujifunza namna ya kujizoea katika hali kujitawala katika muda wa kujitayarisha kwa maisha ya ndoa. Itakuwaje kama mke wako atapata kuwa mgonjwa hata hamwezi kutwaana kimwili? Upendo si ya kujifurahisha tu, lakini unadai kujinyima hata sadaka. Mtu akisema kwamba hawezi kungoja hadi arusi, bora asioe kabisa, maana hawezi kutazamia kwamba atakuwa mwaminifu baadaye. Kristo ametuita tuishi kwa hali ya kujitawala, wala si kwa kutwaana kwa kujifurahisha tu; hii ni tofauti kabisa na yale tuonayo katika television, au yanayoelezwa hata katika dini fulani.

Kutamani kutwaana sio tabia chafu yenyewe; ni kipawa kutoka kwa Mungu. ambacho tunahitaji kumshukuru. Hata hivyo, mtu atakiwa kutawala tamaa yake na bila hata kumjaribu yeyote. Habari ya mtu mzima ambaye anamtumia vibaya mtoto, Yesu alisema, „Yamfaa afungiwe shingoni jiwe la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari“(Mathayo 18:6). Hukumu kali itamngojea mtu wa namna hii. Yeyote awadhulumaye watoto hawezi kuirithi ufalme wa Mungu, isipokuwa anafikia toba la kweli na kuachana kabisa na dhambi yake ( I.Wakorintho 6:9-11). Upendo wa kweli hauwezi kumtendea maovu mtu yeyote.

Wasichana nao wanatakiwa kujitayarisha vema kwa mwenzake wa maisha wakimfuata Yesu. Tabia hiyo sio rahisi wakati ambapo sinema na magazeti bila aibu zinaonyesha picha zitokazo kuzimuni, wala si toka mbinguni. Familia safi ya Kikristo, pia na vikundi vya vijana vyenye kiini cha Yesu zinaweza kusaidia sana, ili polepole vijana wakuze roho, moyo na mwili katika usafi. Bora kabisa msichana ajitoe mapema kwake Yesu. Atakua na kutembea hali analindwa katika majaribu yote. Msichana hana haja ya kumtafuta mume mwenye utajiri au elimu ya juu, lakini awe na uwezo wa kutofautisha moyo mpya unaoishi ndani ya kijana, na kama anajishughulisha katika kazi yake kwa bidii na uaminifu. Matunda ya kiroho ni muhimu zaidi kuliko mvutano wa kiume. Bwana alisema, „Waovu hawatakuwa na amani,“ na hii inaweza kutimizwa katika mazingira ya maisha ya ndoa. Lakini tusijidanganye wenyewe: Nyoka alikutwa hata ndani ya paradiso. Hakuna usalama au amani maishani mwa binadamu bila kumwelekea Yesu na kudumu ndani yake. Yeye ndiye pekee awezaye kutusaidia kushinda majaribu. Kwa vile hakuna hata mmoja kati yetu aishiye bila dhambi, inatupasa kuungama dhambi zetu na makosa kwake Yesu. Unapochelewa kwa kuungama, dhambi itakukumba tena. Umweletee Bwana naye atakulinda haraka. Umkimbilie Yeye kila mara unapozungukwa na majaribu.

Sikukuu ya Arusi inapasa kuongozwa katika jina la Yesu, na ikiwezekana, katika ibada kanisani, kwa kutazamia maisha ya baraka. Fedha, nguo, afya na mali ya kidunia sio kiini cha ndoa, lakini Bwana na Neno lake zinathibitisha neema juu ya neema kwa ajili ya watu wa ndoa wa kimungu. Yesu asema, „Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa“ (Mathayo 6:33). Hata kama kuna shida ya uhanithi au utasa, ndoa inaweza kuwa ya kufanikiwa na heri. Watu wa namna hii wangeweza kupokea baraka ya pekee na hekima tukufu katika kumtumikia Yesu kwa njia mbalimbali. Wangeweza kulea watoto wasio na familia au kufanya kazi za ufadhili kwa ajili ya Bwana. Ikiwa basi, ndoa inaandaliwa bila Mungu Baba, Yesu na Roho yake, ukafiri wa ki-ndoa hata kuachana inatazamiwa na imepangwa hivyo mapema, kwa sababu wasioamini ni mara chache tu wamejifunza kujinyima wala maisha yao ya kujizunguka wenyewe tu. Yeyote atakayeoa kwa muda mfupi tu (mut’a) au kuishi na mke bila mpango kamili, au hata kwa namna ya watatu, basi hajatambua siri za kiroho na za kimaisha ya asili ndani ya mwanaume na mwanamke na anapungukiwa na hofu ya Mungu. Uhuru bila utii wa imani ni mlango wazi kwa ajili ya ukosekano wa kujitawala. Uadilifu ndiyo msingi wa kila ustaarabu, kwa hiyo usimjaribu Bwana Mungu, aliye Mwumbaji wako. Roho Mtakatifu hawezi kuruhusu uchafu, umalaya, nguo za kuvutia uzinzi, mizaha michafu, chakula cha kupita kiasi, ulevi au kutumia madawa ya kulevya. Hayo yote ni dalili za uchakavu, yanayochafua mioyo, kutia sumu akilini na kuharibu miili ya mamilioni ya watu. Ama tunaishi ulimwenguni chini ya utawala wa shetani, aliye mfalme wa dunia hii, au tunaishi ndani ya Kristo, aliye Mwokozi wa pekee anayetuimarisha katika udhaifu wetu. Ulimwengu wetu umepata kuwa na hali ya kusadiki vitu vinavyoonekana tu, wala hauko tayari kuishi kufuatana na thamani za waumini wa Yesu Kristo, waliokwisha kurithi usafi na utakatifu wake.


09.6 - Ndoa kwa msimamo wa Mwislamu

Uislamu umetoa amri za pekee katika Sharia kwa ajili ya ndoa, na unadai kwamba, Ulaya na Waamerika wanaweza kuinuka tu kutoka katika upungufu wao wa uadilifu kwa kukubali Sharia.

Mhamadi aliwaruhusu wafuasi wake wachukue wake hadi wanne. Aliruhusu hata ndoa ya mut’a ambayo ni ya muda mfupi tu inavyokubaliwa , kwa kiasi fulani ya fedha (Sura al-Nisa 4:4,24). Wafuasi wake walikuwa wapigani mashujaa na wafanya biashara wazoefu. Mara nyingi walikuwa mbali na nyumbani kwa muda mrefu na walihitaji kutimiza haja zao za uhusiano wa kutwaana. Kujinyima na kujikana sio mwenendo kwa wanaume katika Uislamu, lakini kwa ajili ya wanawake tu. Mwanzilishi wa Uislamu mwenyewe kihalali aliwaoa wanawake 13, bila hata kutaja wake za kinyumba waliokuwa ni wa kiyahudi, kikristo na wa kipagani.

Karibu katika nchi zote za kiislamu mwanaume anayo haki ya kuachana na mkewe hata bila kutoa sababu. Pia anaweza kumrudia mkewe katika miezi miwili bila kutoa mahari kwa upya, asipotaka kuachana naye. Hata kurudia mara ya pili kuachana na kuchukuana tena ni halali. Lakini Mwislamu akiachana na mkewe mara ya tatu hawezi kumwoa tena, isipokuwa ameolewa na mwanaume mwingine kihalali. Ikiwa huyu mume wa mwisho ameachana naye pia, ndipo anaweza kuolewa na mume wake wa kwanza tena. Je, ni nini inayozunguka akilini mwa mwanamke wa namna hii? Anahesabiwa kuwa kama chombo cha nyumbani kama meza au kabati, wala hahesabiwi kama mshiriki wa ndoa aliye na roho yenye usawa na ya mumewe katika staha, haki au wajibu, ili watu hawa waishi katika umoja wa kiroho na kuweza kushinda magumu ya maisha pamoja.

Mwislamu ni kama mzee mkuu ndani ya familia yake anayeruhusiwa kuwa na wake hadi wanne. Lakini anatakiwa kuwapenda wote kwa usawa. Akitoa zawadi kwa mke mmoja, anatakiwa kutenda yale yale kwa wengine wote. Kama mtoto wa mke mmoja anapata nguo mpya, inampasa anunue nguo mpya kwa watoto wa wake wengine kwenye uthamani ule ule. Kwa ajili ya mambo ya kupunguza gharama Waislamu wengi hawaoi zaidi ya mke mmoja.

Hata hivyo, ndoa ya wake wengi inaendelea kihalali katika nchi zote za kiislamu isipokuwa Uturki na Tunesia. – Mara nyingi mke mwenye umri kuba huondolewa na kupokelewa mwingine mwenye umri mdogo, aliye mzuri zaidi. Basi mwanaume anapoendelea na wake wawili, watatu au wanne, katika familia hizo kuna wivu na uchoyo mwingi. Mhamadi kwa matokeo yake na wake wengi, yeye aliwaeleza wanawake kuwa ni chemchemi ya maovu nyumbani na kutamka pia kwamba hawana akili sana na ufahamu mdogo tu wa mambo ya dini (Masud ibn Hanbal II,373). Pia alimfananisha mwanamke mara nyingine na punda, asiyeweza kubeba mzigo wa familia, na alisema kwamba, taifa inayoongozwa na mwanamke lazima itaharibika.

Kurani na Hadithi zinafundisha kwamba, mwanaume anaruhusiwa kumwadilisha mke wake. Lazima amwonye kwanza (kama anahofia kuasi kwake), ndipa anakataa kulala naye na mwisho anaweza kumpiga mpaka atakapomtii (Sura al-Nisa 4:34).

Ushuhuda wa mwanamke barazani inahesabiwa kuwa nusu ya ushuhuda wa mume. Hivyo neno la mwanaume ni sawa na ushuhuda wa wanawake wawili. Pia mke hupokea sehemu ya nane ya urithi anayoirithi mume wake, ikiwa mume anayo wana wa kiume. Mwana, hata akiwa bado ni mtoto mchanga, hupokea robo. Thamani yake kama mwana tayari ni sawa na mara mbili ya mama yake. Pamoja na hayo, jamaa ya mume wanakuja kabla ya mke pia wakati wa kugawa urithi (Sura al-Nisa 4:7-11).

Watoto wote ni wa upande wa mume peke yake. Mke aliyeachishwa inawezekana apokee pendeleo la kuwalea watoto wake hadi wafikie utu uzima. Kawaida mke haishi peke yake na mume wake, lakini pamoja na familia yake yote, ambapo mama mkwe ni mwenye neno la kwanza na la mwisho. Taratibu kuu ya ndoa ya kiislamu sio umoja wa mume na mke au ushirikiano wao kushinda magumu ya maisha, lakini zaidi ni kuhakikisha kwamba ukoo wa upande wa mume unaendelea. Mke si kitu ila mtumishi mwenye daraja la juu kidogo kwa mume. Kazi yake ni kuzaa watoto wa kiume wengi kwa ajili ya kabila lao. Maongozi yake yanaongezeka kadiri anavyozaa watoto wa kiume wengi. Lakini akizaa wasichana, wanasema, “Lo, ni aibu gani hiyo!”

Ikiwa mwanamke aliyeolewa au msichana anakamatwa katika uasherati, Mhamadi ameagiza akwaruzwe mara mia na kikoto (Sura al-Nur 24:3) au apigwe kwa mawe hadi kufa. Siku fulani walimletea Mhamadi mwanamke aliyekuwa na mimba kutokana na mgeni. Alimtuma huyu mwanamke aodoke na arudi mara baada ya kuzaa mtoto wake. Ndipo akaagiza mtoto wake achukuliwe, na yeye apigwe kwa mawe afe mara nje ya nyumba yake. Jinsi ilivyo kubwa mno utofauti kati ya Mhamadi na Yesu ambaye, kutokana na upendo wake wa ki-sadaka, alijitwisha dhambi za waasherati juu yake mwenyewe na kufa kwa niaba yao. Uislamu haumtambui mpatanishi katika hukumu ya Mungu. Ndiyo maana Mwislamu hawezi kumsamehe yeyote makosa yake, lakini inampasa alipize kisasi bila huruma.

Kwa vile uasherati wa wazi ni ya hatari katika Uislamu, haitokei mara nyingi. Hata hivyo sheria ya kiislamu inamruhusu mwanaume kutenda uzinzi kwa namna ya halali. Wakati wowote Mwislamu aweza kuwafukuza wake zake na kumwoa mwingine mwenye umri mdogo. Ingawa nchi kadha za kiislamu zinakataza kuoa wake wengi, roho ile ya Uislamu bado inatawala ndani ya wanaume na wanawake.

Heshima ya chini ya wanawake ndani ya Uislamu inaendelea hadi katika paradise. Mhamadi alisema, „Mwenyeji wa chini katika paradiso ni wanawake.“ Ila wanaume wanangojea kwa hamu anasa mbalimbali, hasa kuwa na makumi ya wanawali ndani ya paradiso, wanaoendelea kuwa mabikira hata baada ya waume wao wamelala nao ndani ya vivuli vya giza. Pia na vijana wa kufurahisha wanapatikana kwa waislamu katika paradiso. Kuhusu matazamio ya mbeleni kwa wanawake Mhamadi alisema, “Nilipoonyeshwa jehanumu, naliona sehemu ya tisini kwa mia ya wale waliowaka moto mle walikuwa ni wanawake.“

Paradiso ya Yesu Kristo ni tofauti kabisa. Mbinguni wafuasi wake wanao utukufu, sawa na malaika wa Mungu, ambao hawaoi wala kuolewa. Ufalme wa Mungu sio kula na kunywa au maisha ya ndoa, lakini upendo wa kiroho, furaha na amani katika nguvu ya Roho Mtakatifu. Paradiso ya kweli sio ya ulimwengu huu. Kufananishwa na mafunuo ya Yesu, je, yeyote ataweza kufikiria Kurani kuwa msingi wa ufunuo tukufu? Inategemea hali ya kujisifu kwa mazoea ya kiume na utawala wao, na ni chini sana ya kawaida ya Agano la Kale na la Agano Jipya.


09.7 - Wito kwa Kuungama (Kutubu)

Wakristo tusiwaangalie Waislamu kutoka kwa juu. Kuna uhuru usio wa kibiblia katika nchi nyingi za Magharibi siku hizi, na kuna kiasi kikubwa sana za ndoa kuachana kule Marekani na Ulaya. Hali hii inaharibu maisha katika ulinzi kwa watoto wengi, wanaotoroka kutoka nyumbabi palipoharibika. Tunahangaishwa kwa njia za kuendesha elimu kuhusu hali ya kuwa kiume au kike (sex) mashuleni. Jinsi picha zilivyo za kuchukiza na kuaibisha ndani ya magazeti, magazines, kwenye video na TV. Na ni wazazi wachache tu wanaoteta kuhusu mambo hayo!

Kutokuwa na taratibu ni kwa sababu ya upungufu wa kicho cha Mungu. Wapiga picha hapo Ulaya wametayarisha njia vizuri sana kwa ajili ya kila namna ya uchafu inayowezekana. Mwanguko kutoka kwa ushirikiano na Mungu umeumba fujo katika tabia ya kutwaana. Vidonge vya kuzuia mimba vinaruhusu watu kutimiza tamaa bila mipaka. Pamoja na hayo, kutumia condom haijasimamisha AIDS. Hii ndiyo malipo mabaya kwa yeyote asiye mwaminifu kwa mke wake, pia kwa waume kwa waume, wake kwa wake, wamalaya au kwa yeyote anayetumia madawa. Paulo kwa Warumi 1:24 ameandika, “Kwa ajili ya hayo Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima miili yao.“ Hukumu ya Mungu haiweki utofauti kati ya Mwislamu, Myahudi au Mkristo. Kwa kuangalia tena kwa jumla amri ile, „Usizini“, inamaanisha kwamba mamilioni ya watu wanajihatarisha kutokana na dhambi za kutwaana. Maana ya ule mstari unaosema, „Mshahara wa dhambi na mauti“ siku hizi inakuwa wazi zaidi kuliko hapo nyuma.

Bahati mbaya, watu wasio na hatia wanaweza kushikwa na AIDS kwa njia ya kuhitaji damu ya mtu mwingine. Kwa sababu hiyo haifai kumhukumu mtu aliye na ugonjwa huo. Mungu pekee afahamu maisha yaliyopita kwa kila mmoja wetu. Sisi hatuwi bora kuliko mtu yeyote aliyekamatwa katika uasherati. Yesu pekee ajua yaliyomo mioyoni mwetu anaposema, „Kwa maana moyoni hutoka mawazo mabaya, uuaji, uzinzi, uasherati; wivu, ushuhuda wa uongo na matukano“ (Mathayo 15:19). Hatuhitaji kuelewa njia salama zaidi ya kuzuia AIDS, lakini kila mmojawetu anahitaji moyo safi, roho iliyotakata na mawazo mapya. Mfalme Daudi, aliyeanguka katika uasherati na kuua alipojiachilia kwa tamaa zake, bado aweza kutufundisha kuomba, „Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.Usinitenge na uso wako, wala roho yako mtakatifu usiniondolee“ (Zaburi 51:10+11).

Kuomba maneno hayo kwa uaminifu na kuungama dhambi zetu kwake Yesu inatuhakikishia itiko lake tukufu, „Jipe moyo mkuu, mwanangu, umesamehewa dhambi zako“ (Mathayo 9:2b na Luka 7:48). Bwana wa utakatifu anatuhakikishia nguvu ya Roho yake Mtakatifu kuongoza katika maisha safi pamoja na kutusamehe dhambi zetu zote. Yesu hatatuacha peke yetu katika majaribu yetu, lakini yu tayari kutuimarisha, ili tuyashinde katika jina lake.

www.Waters-of-Life.net

Page last modified on August 01, 2017, at 01:56 PM | powered by PmWiki (pmwiki-2.3.3)