Waters of Life

Biblical Studies in Multiple Languages

Search in "Kiswahili":
Home -- Kiswahili -- Romans - 001 (Introduction)
This page in: -- Afrikaans -- Arabic -- Armenian -- Azeri -- Bengali -- Bulgarian -- Cebuano -- Chinese -- English -- French -- Georgian -- Greek -- Hausa -- Hebrew -- Hindi -- Igbo -- Indonesian -- Javanese -- KISWAHILI -- Malayalam -- Polish -- Portuguese -- Russian -- Serbian -- Somali -- Spanish -- Tamil -- Telugu -- Turkish -- Urdu? -- Yiddish -- Yoruba

Next Lesson

WARUMI - BWANA NDIYE HAKI au UADILIFU WETU
Masomo kuhusu Barua ya Paulo kwa Warumi

UTANGULIZI


Utangulizi kwa Barua ya Paulo kwa Warumi

Mojawapo katika zawadi kuu kutoka kwa Kristo Bwana, aliyefufuka kutoka kwa wafu, aliyeitoa kwa kanisa lake kwa wakati wote, ndiyo barua muhimu aliyemwongoza Paulo, mtume wake, aiandike kwa Warumi, watu walioishi katika jiji kuu la Rumi.

Sababu na kusudi la Barua hili

Wakati wowote mtume wa watu wa mataifa alikamilisha mahubiri yake upande wa Mashariki ya Kati na sehemu za Ugriki (Uyunani) wakati wa safari zake tatu za umissionari. Katika muda wa hizi safari za umissionari aliweka misingi ya makanisa hai kwenye miji mikuu, akawaimarisha waumini katika huduma ya upendo, akawaamuru wazee wa kanisa, wachungaji na maaskofu kwa ajili ya washiriki ndani ya makanisa. Ndipo akaona kwamba, huduma yake katika maeneo ya mashariki ya Bahari ya Kati ilikuwa imekamilika. Basi, akaelekea upande wa magharibi, ili kuanzisha Ufalme wa Kristo katika nchi za Ufaransa na Spania (Warumi 15:22-24).

Kwa kupatanisha na mipango hii, aliandika barua yake maarufu kwa washiriki wa kanisa la Rumi, ili aimarishe tumaini lao ndani yake, akiwahakikishia kwamba yeye ni mtume wa Kristo kwa Mataifa yote kwa njia ya kuchunguza kwa uangalifu Injili aliyokabidhiwa mikononi mwake. Alijaribu kugusa mioyo yao, ili wao nao washiriki katika safari yake ya umissionari kuelekea magharibi zaidi, jinsi kanisa la Antiokia la Shamu lilivyoimarisha safari zake, mahubiri na mateso yake kwa njia ya maombi yao kwa uaminifu. Kwa sababu hiyo barua kwa Warumi inakuwa na mafunzo ya kutangulia kwa kusudi la kulisadikisha kanisa liimarike katika imani ya kweli, na pia kulitayarisha kwa ajili ya kuhubiri kwa Mataifa wakishirikiana na huduma yake Paulo.

Nani alianzisha Kanisa kule Rumi?

Si Paulo wala si Petro, wala si mtume yeyote mwingine, na pia sio mzee mwingine anayejulikana sana aliyeanzisha kanisa la Rumi. Hata hivyo, ilitendeka kwa njia ya watu walioenda kuhiji na kutokea kwenye nchi takatifu wakati wa Pentekoste, ambapo Kristo alimwaga Roho Mtakatifu juu ya watu waliokuwa na sala za kuungama. Ndimi zao zilijazwa na mambo makuu ya yule Mwenye Enzi, na kufuatana na hayo wakarudi kwenye miji yao mikuu wakashuhudia katika mikutano yao habari ya Mwenye Enzi aliyesulibiwa. Walizungumza na marafiki yao ya kiyahudi na ya Mataifa mengine habari ya wokovu wake Kristo, nao wakaanzisha vikundi manyumbani mwao kwa ajili ya kuchunguza utabiri wa Agano la Kale kumhusu Kristo.

Wakati wa safari zake katika Asia Ndogo na Ugriki, Paulo mara kwa mara alikutana na waumini kutoka Rumi, na hasa Wayahudi walipofukuzwa toka Rumi wakati wa utawala wa Kaisari Klaudio mwaka 54 AD (Matendo ya Mitume 18:2). Paulo alijibidiisha kupata uhusiano ya binafsi na kanisa la Rumi, pia na kuwagawia vipawa vya Roho Mtakatifu vilivyofanya kazi ndani yake. Hakufikiri kwamba kukaa muda mrefu kwenye mji mkuu wa ulimwengu kulihitajika, maana alitambua kule kuna kanisa lenye uhai na la kujitegemea.. Badala yake alitaka aende zake pamoja na ushirikiano na ndugu katika Bwana, ili aeneze Injili ya wokovu katika maeneo yaliyofungwa bado.

Nani aliandika barua hii? Lini? Na wapi?

Mtume Paulo ndiye aliyeiandika barua hii mwaka 58 A.D. (baada ya Kristo), wakati alipokaa kwenye nyumba ya Gaius mjini Korintho, na ndani yake alijumlisha mambo aliyoyaona na kuonja ya kiroho, pia na mafundisho ya kitume. Hakuna awezaye kuandika jinsi Paulo alivyofanya katika barua hii, maana Kristo biafsi aliye hai na mwenye utukufu alisimama katika njia yake, alipokuwa mwenye shauku kwa ajili ya Sheria ya Wayahudi (Torati), na kutafuta namna ya kuwadhulumu kwa vikali Wakristo wa Dameski. Na pale nuru ile tukufu ilipomwingilia, alitambua kweli ile kuu kwamba, Yesu wa Nazareti, aliyekuwa amedharauliwa, yu hai tena, naye ndiye Bwana wa utukufu, wala hakuharibika kaburini baada ya kusulibiwa kwake. Badala yake Yesu alishinda mauti, na kweli kabisa amefufuka, hivi akithibitisha kwamba, ndiye Mwenye Enzi anayetawala yote. Hapo basi Paulo alitambua kwamba, Mwana wa Mungu hakumhukumu au kumharibu yeye aliyekuwa anamdhulumu, bali alimhurumia na kumwita kufanya kazi yake ya umissionari; na hilo si kwa sababu alikuwa akifaa sana, lakini kwa ajili ya neema yake tu. Kwa sababu hiyo huyu Paulo mwenye shauku na kicho akavunjwa-vunjwa na kudhikishwa. Akaamini ndani ya neema ya Mungu na kiini cha haki mpya iliyopatikana. Hapo hakuendelea kutegemea uwezo wake wa kibinadamu kufuatana na Sheria. Badala yake akainuka na kuelekea ulimwenguni kote, akiwa mtumishi wa upendo tukufu wa Kristo, akiwaita wote waliodanganyika na kuchafuka wakubali kupokea upatanisho na Mungu.

Zipi ni mitindo ya kipekee katika barua hii?

Paulo alikusudia kuweka wazi kabisa badiliko lake la kidini kwa kila mshiriki wa kanisa la Rumi. Hata hivyo, kwa kusudi hilo, hakuandika kitabu chenye lugha safi na kupendezesha, wala si mahojiano marefu ya kulinganisha mambo. Hivyo aliandika barua yenye lugha rahisi na ya wazi kabisa, na ndani yake kujibu maswali ambayo alitazamia yataulizwa na Wayahudi na Warumi. Paulo aliandikisha barua yake kwa Tertio, ndugu yake katika Bwana, akiwafikiria mawazoni mwake wale aliyewaandikia. Mahali fulani katika barua hii aliwaandikia hasa wale waliopata kuamini hivi karibuni tu, akiwasemea hali yao ya juu juu kuhusu utakatifu wa Mungu wa kuweza kuwatakasa. Ndipo aliwavuta wale wenye kuvunjika kiroho waje kwenye imani hai, inayopatikana katika upatanisho kamili ndani ya Kristo, aliye tumaini la pekee kwa wanadamu. Mahali pengine tena aliwatikisa wanasheria wenye kiburi, naye akavunja haki zao za binafsi, akiwaonyesha uchafu wao na walivyopotoka kabisa, ndipo akawaonyesha jinsi walivyoweza kubarikiwa kwa imani nyenyekevu katika huduma ya upendo wa Mungu, huku wakimtii Roho Mtakatifu. Ilivyopasa katika barua yake, mtume aliunganisha mahubiri yenye shabaha nzito pamoja na mafundisho ya kawaida kwa upole.Hakuwaandikia kundi la watu wa pekee tu, lakini aina zote za wasikilizaji; watu wa Mataifa na Wayahudi, vijana na wazee, wasomi na wasiokuwa na elimu, watumwa na watu huru, pia na wanaume na wanawake. Barua kwa Warumi hadi leo ni mojawapo katika mafundisho makuu ndani ya Ukristo, jinsi Dr. Martin Luther alivyoshuhudia ndani ya tamko lake fulani: „Kitabu hiki ni sehemu kuu ndani ya Agano Jipya, na Injili iliyo safi, inayostahili kujifunzwa kwa moyo na kila Mkristo. Iambatishwe kila siku kuwa hazina ya kiroho kwa moyo wa kila mtu, kwa sababu tunagundua kwa wingi ndani ya barua hii yale yanayopaswa kufahamika na kila mwumini: Sheria na Injili, dhambi na hukumu yake, neema na imani, haki na ukweli, Kristo na Mungu, matendo mema na upendo, tumaini na pia Msalaba. Pia tunatambulishwa namna ya kuenenda na kila mtu, bila kujali kicho au madhambi yake, uwezo au udhaifu wake, mwenye upole au ukorofi aliyo nayo; na pia twafundishwa namna ya kujitunza wenyewe. Basi, natoa shauri kwa Wakristo wote wajibidiishe kujifunza yaliyomo.“

Mpendwa ndugu, kama unatafuta somo la muhimu na la kukufundisha ndani ya imani yako, basi tafakari sana na kuchunguza barua hii kwa Warumi na kuisoma kwa bidii. Maana ni kama chuo kikuu cha Mungu kilichojaa elimu ya kiroho, nguvu na enzi. Ndipo pia Kristo atakuondolea darau lako na hali yako ya kujitegemea, naye atakujenga ndani ya haki kamili, ili upate kuwa mtumishi mwenye nguvu katika kutumia upendo tukufu na kukua katika imani siku hadi siku.

Mchanganuo wa Barua kwa Warumi

Warumi 1:1-17 -- Ufasaha wa mwandishi aliyeandikia kanisa la Rumi. Mbaraka wa kitume. Toleo la haki ya Mungu kama alama kuu ya barua yake.

SEHEMU YA 1 - HAKI YA MUNGU INATUHESABIA KUWA WENYE HAKI

Warumi 1:18 - 3:23 -- Sote tu wenye dhambi, na itampasa Mungu kutupatia adhabu kufuatana na sheria, inayovunja nia ya kiburi chetu.
Warumi 3:24 - 4:25 -- Mungu katika uhuru yake anawahesabia kuwa wenye haki wanadamu wote kwa kazi ya ukombozi wa Kristo, ikiwa wataamini ndani yake.
Warumi 5:01 - 8:39 -- Roho wa Bwana huishi na kutawala ndani ya waumini na kuwapatia tumaini na ushindi juu ya dhambi, nao wanatembea katika nguvu ya Roho, wakiwa huru na sheria.

SEHEMU YA 2 - HAKI YA MUNGU NDANI YA HISTORIA YA WATU

Warumi 9:1 - 11:36 -- Munugu huendelea kuwa na haki, mbali na watu wa Agano la Kale waliokataa neema yake.

SEHEMU YA 3 - HAKI YA MUNGU NDANI YA MAISHA YA KILA SIKU

Warumi 12:1 - 16:27 -- Imani ya kweli inabadilisha kabisa tabia na maisha yetu tuwe na matendo ya upendo na ya kujitoa sisi kwa sisi.

Kweli barua hii si rahisi kuichunguza na kuelewa. Itakudai kuwa na uchunguzi kwa uangalifu, pia na maombi, na kuzingatia sana mawazoni mwako, ili uweze kufurahia baraka zake; pia uungame kwa uaminifu, ufanywe upya rohoni mwako, na upate kuona mafafanuzi mapya ya uhai ndani ya Kristo. Jinsi barua hii haikupeleka ulegevu wa kiroho kwa Warumi, badala yake kuwatayarisha kwa kazi ya kuhubiri katika maeneo yao na hata katika nchi zingine, ndivyo Kristo anakukaribisha na wewe ujazwe na neema yake, ili aweze kukutuma pamoja na ndugu zako waaminifu, mweze kwenda kwa watu wasio na upendo wala tumaini. Basi, usikilize, uombe, na ndipo uende.

MASWALI:

  1. Zipi ni kusudi na mwisho wa Barua kwa Warumi?
  2. Ni nani aliyeanzisha Kanisa la Rumi?
  3. Nani aliyeiandika barua hii? Na wapi? Na lini?
  4. Paulo alitumia mitindo gani katika kuiandika barua hii?
  5. Ipi ni mpangilio wa barua hii?

www.Waters-of-Life.net

Page last modified on November 14, 2022, at 01:44 PM | powered by PmWiki (pmwiki-2.3.3)